
UBALOZI WA KANADA NCHINI TANZANIA kupitia kitengo cha Mashirikiano imepongeza hatua zilizofikiwa na watekelezaji wa mradi wa kuwawezesha wanawake na uongozi katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi (Zanzadapt) wakiwemo Jumuia ya uhifadhi wa misitu Pemba (CFP), Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania,ZANZIBAR, (TAMWA_ZANZIBAR) pamoja na Jumuia ya misitu Kimataifa (CFI) .
Pongezi hizo zimetolewa na Mkuu wa Mashirikiano kutoka ubalozi wa Canada Carol Mundle katika mkutano maalum uliowashirikisha wadau wanaotekeleza mradi uliofanyika katika ukumbi wa SUNSET Wesha chake chake Pemba.
Carol amesema kuwepo kwa mradi wa Zanzadapt kumewawezesha wanawake kushika nafasi za uongozi katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi jambo ambalo linaleta mabadiliko kwa wanawake wa Zanzibar.
Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Mali Asili na Mifugo Zanzibar, Ali Khamis Juma amesema kwa sasa Wizara imepanga mikakati mbali mbali kwa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ikiwemo kuongeza wataalam wa kilimo kila shehia kwa kutoa elimu kwa wakulima ili kulima kilimo chenye tija.
Mapema Mkurugenzi wa Jumuiya ya Misitu Pemba (CFI) Mbarouk Mussa Omar amesema wametoa elimu kwa wakulima viongozi, (TOTs) 50 kwa Unguja na Pemba kupitia mradi wa Zanzadapt kwa lengo la kutoa elimu kwa jamii kutumia fursa ya kujiongezea kipato kupitia kilimo.
Mkuu wa Mawasiliano Chama cha Waandishi Wahabari Wanawake Tanzania Zanzibar, TAMWA ZNZ, Sophia Ngalapi amesema kupitia mradi huo TAMWA ZNZ Imetoa mafunzo kwa waandishi wahabari 30 na wahariri 20 ili kuandika habari zinazohusu wanawake na uongozi katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ambapo tokea kuanza kwa mradi huo November 2023 hadi sasa habari 118 zimeripotiwa kutoka vyombo mbali mbali vya habari ikiwemo radio, Magazeti, TV na mitandao ya kijamii.
Nae Mtaalam wa masuala ya Jinsia kutoka CFP, Sada Juma Segeja akiwasilisha ripoti ya mradi katika kipengele kinachohusu usawa wa jinsia amesema katika utekelezaji wa mradi wa Zanzadapt umelenga kuwanufaisha wananchi 2,191 ambapo wanawake ni 81%, walioshika nafasi za uongozi ambao ni wakulima viongozi 45% na 23% ni wanawake waliojiongezea kipato.
Mkutano huo wa kuwasilisha ripoti za utekelezaji wa mradi ZANZ- ADAPT uliowashirikisha wadau kutoka wizara ya Kilimo ,Umwagiliaji ,Maliasili na Mifugo ,Wizara ya Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto, Wizara ya uchumi wa Bluu na Uvuvi Iidara ya misitu Pemba , wakulima viongozi pamoja na viongozi wa shehia ambazo zinahusika na mradi huo.
Awali mkutano huo ulianza na ziara ya siku moja kutembelea baadhi ya maeneo yanayotekelezwa na mradi huo katika Wilaya ya Wete, ambapo ni Shehia ya Kiuyu na Mchangamdogo kuzungumza na wanufaika pamoja na kujionea athari na mafanikio ya mradi huo kisiwani Pemba.
MWISHO